Basi la Timu ya Taifa ya Tanzania limekombolewa na
TFF
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF),
limefanikiwa kulikomboa basi la timu ya soka la wanaume ya Tanzania, ‘Taifa Stars,’ huku likikiri kupata usumbufu
mkubwa wa deni la kurithi la shilingi mil. 140 lililosababisha kukamatwa kwa
chombo hicho ghali.
Basi kubwa la Taifa Stars aina ya
Yutong lililotolewa na wadhamini wa Taifa Stars, Kampuni ya Bia Tanzania (TBL)
kupitia kinywaji cha Kilimanjaro Premium Lager, lilikamatwa katikati ya mwaka
jana kwa agizo la Mahakama, ambapo TFF ilitanguliza sh. Mil 70.
Akizungumza na mwandishi wetu jijini
Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa TFF, Mwesigwa Selestine, amesema harakati
mbalimbali za ndani na nje ya Mahakama, zimefanikisha kukombolewa kwa basi hilo
na sasa liko mikononi mwao tayari.
“Hili ni suala la kisera na
lilipaswa kuzungumzwa na Rais wa TFF, lakini kifupi ni kwamba tumemaliza kulipa
deni husika ambalo TFF yetu ilirithi kutoka kwa TFF iliyopita, hivyo
tumelikomboa rasmi basi hilo na liko mikononi mwetu,” Amesema Mwesigwa.
Mwesigwa amesema kuwa, kimsingi deni
hilo liliwapa wakati mgumu na hawakuwa na njia ya kutolilipa baada ya kulirithi
na kwamba liliwaumbua vya kutosha, ingawa wanashukuru kwa jitihada zao za
kulikomboa kuzaa matunda.
Source: hivisasa.co.tz
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni