Kipa wa zamani wa Simba na timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ Juma Kaseja, leo alikuwa kivutio kikubwa kwa wachezaji wa Simaba waliokuwa wakifanya mazoezi kwenye uwanja wa Chuo kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).
Mara baada ya kocha mkuu wa ‘Wekundu wa Msimbazi’ Goran Kopunovic kuhitimisha ‘program’ ya mazoezi kwa siku ya leo, wachezaji wa Simba walikwenda kumvamia kipa huyo mkongwe nchini na kuanza kumsalimia huku wengine wakimtania.
Kaseja alifika uwanjani hapo akiongozana na baadhi ya wachezaji wa timu ya Taifa ya wanawake ‘Twiga Stars’ kwa lengo la kufanya mazoezi lakini ilibidi asalimiane na wachezaji wenzake wa zamani kabla hajaingia uwanjani kuanza kujifua.
Kaseja alisajiliwa na klabu ya Yanga baada ya kutemwa na Simba lakini alishindwa kupata namba ya kudumu kwenye kikosi hicho chenye maskani yake kwenye makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani. Kaseja aliamua kutimka Yanga bila ruhusa maalum baada ya jina lake kutoorodheshwa kwenye orodha ya wachezaji watakaotumiwa na Yanga kwenye michuano ya kombe la shirikisho barani Afrika.
Licha ya kuondoka kwake lakini bado anamkataba na Yanga na timu hiyo tayari imeshamfungulia kesi kwenye mahakama ya kazi ikimlalamikia mchezaji huyo kuvunja mkataba na kutoroka kwenye klabu hiyo bila taarifa rasmi wakati anajua yeye ni mchezaji halali wa klabu hiyo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni