London, England
MICHEZO sita mpaka nane imebaki ya Ligi Kuu England ‘Premier’ kabla ya ligi hiyo haijafikia tamati msimu huu wa 2015/16. Msimamo wa ligi hiyo unaonesha Leicester City ipo kileleni huku ikipewa nafasi kubwa ya kuwa bingwa.
Leicester inaongoza ikiwa na pointi 69 ambazo ni saba zaidi ya timu inayoifuatia kwa ukaribu, Tottenham Hotspur, huku wakiiacha Arsenal inayoshika nafasi ya tatu kwa pointi 11.
Kwa hali ilivyo, Leicester wanatakiwa kukusanya pointi 12 katika michezo yao sita iliyosalia ili waweze kuwa mabingwa. Timu hiyo ina jopo la watu wengi wanaochangia mafanikio hayo, lakini leo tutakufahamisha wachache tu.
Kocha mkuu wa kikosi hicho, Claudio Ranieri amekuwa nguzo mojawapo ya mafanikio ndani ya timu hiyo msimu huu. Muitaliano huyo ameweza kuwa na mbinu za ushindi kila wanaposhuka dimbani hasa tangu pale walipoanza kujiona wanaweza kuwa mabingwa.
Kuhusu kuelekea kulitwaa taji la ligi hiyo, Ranieri anasema: "Siwezi kusema sana kuhusu hilo, bali watu wanatakiwa kuamini kwa kile tunachokifanya.
" “Huu unaweza kuwa msimu wa maajabu kwetu na sidhani kama msimu ujao utakuwa kama hivi, kwa sasa tunajaribu kufanya kila tuwezalo, hivyo tunatakiwa kuwa makini kipindi hiki." Morgan na Huth Morgan ni nahodha wa kikosi hicho , anaunda safu kali ya ulinzi sambamba na, Robert Huth.
Morgan ameweza kucheza katika kila mchezo wa timu hiyo msimu huu na wikiendi iliyopita aliifungia timu yake hiyo bao muhimu dhidi ya Southampton katika ushindi walioupata wa bao 1-0.
Kuanzia misimu miwili nyuma katika Premier mpaka leo, hakuna beki aliyezuia mashambulizi mara nyingi kuliko Morgan. Morgan na Huth kwa pamoja wamecheza mechi 19 za Premier bila ya kuruhusu bao tangu timu hiyo ilipoepuka janga la kushuka daraja msimu uliopita.
Kanté Kiungo mkabaji, N'Golo Kanté, alijiunga na kikosi hicho mwanzoni mwa msimu huu akitokea timu ya Caen ya Ligi Daraja la Pili Ufaransa.
Amekuwa akiwavuruga wapinzani hasa kwenye nafasi yake anayoimudu, pia msimu huu aliwahi kufunga bao la ushindi kwa timu yake walipoichapa Watford 2–1, Novemba 7, mwaka jana.
Hakuna aliyekuwa akiamini kama mchezaji kutoka Ligi Daraja la Pili Ufaransa kama atakuja kuwa hatari kwenye Premier ligi ambayo wachezaji wengi wamekuwa wakishindwa kuwika.
Kante amefanikiwa hilo na amekuwa gumzo kila anapokuwa uwanjani. Mahrez Kiungo Mualgeria, Riyad Mahrez amekuwa chachu kubwa kwa kusaidiana na Jamie Vardy kwenye safu ya ushambuliaji. Mabeki hupata shida sana kumkaba akikaribia eneo la 18 la timu pinzani.
Mguu wake wa kushoto anautumia vyema kuwahadaa mabeki na mara kadhaa hufunga ama kutoa pasi za mabao kwa wenzake. Mpaka sasa amefunga mabao 16 na kutoa pasi za mabao 12.
Okazaki Desemba 19, mwaka jana, Shinji Okazaki alifanikiwa kufunga bao la kwanza na la tatu kwa timu hiyo katika ushindi wa ligi walioupata wa mabao 3-2 dhidi ya Everton huku akitoa pasi ya bao la pili kwa Jamie Vardy.
Ushindi huo ukawafanya kukaa kileleni mpaka kinapita kipindi cha Sikukuu ya Krisimasi.
Kuna dhana kwamba katika Premier, timu ikiwa kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo kwa kipindi cha Krisimasi, basi ina nafasi kubwa ya kuwa bingwa msimu huo, kwa maana hiyo kama Leicester itafanikiwa kuwa bingwa, basi Okazaki ndiye mtu wa kwanza kutajwa kati ya wale waliotengeneza njia ya mafanikio.
Vardy Jamie Vardy ana mabao 19 ya ligi msimu huu na amekuwa akifunga mara kwa mara. Anatazamwa kwa jicho la tatu ndani ya kikosi hicho na anatajwa kuwa ndiye straika anayeibeba zaidi timu hiyo hasa katika mechi ngumu kwani kama hajashinda basi anatengeneza nafasi ya kufunga kwa wenzake.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni