Matola (kulia) alicheza soka siku ya Simba Day
Simbasports.co.tz
jana ilipata nafasi ya kuongea na kocha msaidizi wa Timu ya Simba,
Seleman Matola kuhusu maendeleo ya timu, ushauri kwa kikosi kizima
pamoja na Uongozi.
Haya ndio yalikuwa mahojiano yao na Matola:-
Simbasports.co.tz: Habari yako Matola?
Matola:
Namshukuru Mungu mimi nipo salama kabisa, naendelea vizuri na kazi
zangu za kila siku katika kushirikiana na kocha Dylan Kerr kuifundisha
timu yetu ya Simba.
Simbasports.co.tz: Vipi unaonaje kikosi chako cha Simba katika kujiandaa na ligi kuu Tanzania Bara?
Matola:
kikosi changu kipo vizuri sana tena sana, kama ambavyo unaona mpaka
sasa hatujapoteza hata mechi moja ya kirafiki tangu tuanze kufanya
mazoezi ya kujitayarisha na kuanza kwa ligi. Hili ni jambo kubwa na la
kutia faraja sana kuona kuwa wachezaji wanafuata mafundisho
tunayowapatia sisi kama makocha ili kuweza kuupata ushindi katika
michezo yetu yote.
Simbasports.co.tz:
Kwenye mchezo wa kimataifa wa kirafiki kati ya Simba na URA tuliona
kuwa Simba ikicheza ikiwa na wachezaji 9 uwanjani na kuweza kushinda,
kwa nini mliamua kuchezesha wachezaji 9 baada ya mchezaji Peter
Mwalyanzi kuumia?
Matola:
Unajua kwenye mpira kuna mambo mengi sana yanaweza kutokea, mchezaji
kuumia, mchezaji kupewa kadi nyekundu hata mchezaji kuwa nje ya mchezo
ni kawaida, hivyo ni lazima kuijenga timu ikijua kuwa hata wakiwa
pungufu bado wanatakiwa kuwa na ari ya ushindi na ndicho kilichotokea
kwenye mechi ya Jumamosi na Klabu ya URA ambapo tulipata goli la pili
tukiwa tunacheza wachezaji 9.
Simbasports.co.tz: Je una ushauri gani kwa wachezaji?
Matola:
Kwanza ni kuendeleza usikivu wanaouonesha kwa Makocha na Viongozi wetu
wa Simba kwa ujumla, kufanya mazoezi ya kutosha pamoja na kujituma
zaidi.
Simbasorts.co.tz: Una ushauri gani kwa Viongozi wa Simba?
Matola:
Ushauri wangu ni uleule kila siku viongozi ni lazima wadumishe
mshikamano walionao sasa hivi, ni lazima wawe na umoja na kuendelea kuwa
karibu na timu yao.
Kocha msaidizi Matola amezaliwa tarehe 24 – 4 – 1978 na aliichezea Simba kwa mafanikio makubwa sana katika miaka ya 2000.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni